Siku
mbili baada ya baadhi ya wabunge kudaiwa kuhusika katika vitendo vya
rushwa, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa
(Takukuru), Valentino Mlowola amesema taasisi yake inawahoji wote
waliotajwa kuhusika na tuhuma hizo.
Hatua hiyo imekuja kutokana na tuhuma za rushwa dhidi ya wabunge wa
baadhi ya kamati za Bunge na kusababisha baadhi yao kuomba kujiuzulu
ujumbe wakishinikiza uchunguzi ufanyike ili waliohusika wawekwe
hadharani na kuchukuliwa hatua.
Mkuu huyo wa zamani wa Intelijensia ya jinai katika Jeshi la Polisi
alisema:“Sisi tunachunguza tuhuma zote zinazohusiana na rushwa, kwa
maana hiyo tunawachunguza wabunge wote waliotajwa.”
Alisema uchunguzi huo unakwenda zaidi hadi kuyagusa mashirika ya umma
kwa kuwa lengo ni kushughulikia kashfa ambayo inaweza kuharibu heshima
ya Bunge.
Mashirika ya umma yaliyoguswa katika tuhuma hizo ni Shirika la Umeme
Tanzania (Tanesco), Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), Mfuko wa Taifa wa
Bima ya Afya (NHIF) na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji
(Ewura).
Alipoulizwa uchunguzi huo utakamilika lini, alisema hawezi kubashiri
kwa kuwa hilo ni suala la utendaji ambalo linafuata sheria na taratibu.
Wabunge wafunguka
Wakati Takukuru ikichukua hatua hiyo, wabunge watano waliokumbwa na
mabadiliko ya kuhamishwa kamati yaliyosababisha baadhi yao kupoteza
nyadhifa zao huku yakielezwa kuwa ni ya kawaida, wamefunguka kuhusu
uamuzi huo huku baadhi yao wakiushangaa.
Waliopoteza nafasi zao kutokana na mabadiliko hayo ni Richard Ndassa,
ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uwekezaji na Mitaji (PIC), Mary
Mwanjelwa (Ardhi, Maliasili na Mazingira), Martha Mlata (Nishati na
Madini).
Waliovuliwa umakamu mwenyekiti ni Dk Raphael Chegeni (Huduma za
Maendeleo ya Jamii) na Kangi Lugola (Hesabu za Serikali za Mitaa).
Mwanjelwa alisema inasikitisha na kushangaza kusikia tuhuma zikitolewa
kwenye vyombo vya habari na baadaye kuona mabadiliko ya kamati hizo
yakifanyika.
Alisema kwa sasa bado anatafakari: “Lakini kwa kuwa Spika ndiyo amepewa
mamlaka kwa mujibu wa kanuni za Bunge basi huwezi kupinga,” alisema.
Mlata alisema kwa sasa hawezi kuzungumza kauli yoyote kabla ya kuonana na Spika.
Ndasa alisema Serikali ina mkono mrefu wa kufuatilia na kuchunguza
tuhuma hizo ili kujiridhisha huku akisema mabadiliko yaliyofanyika ni
kawaida na yapo ndani ya mamlaka ya Bunge na hawezi kuhusisha mabadiliko
hayo na tuhuma za rushwa.
Chegeni alikubaliana na mabadiliko hayo huku akibainisha kuwapo kwa kundi la watu wanaojaribu kuchafua taswira ya kamati yake.
No comments:
Post a Comment